Saturday, April 9, 2016

SEHEMU YA TISA

Shuta alimhimiza dereva wake aendeshe gari lake kwa kasi. Dereva alivurumisha gari kwa kasi ajabu. Magurudumu yakiwa hayaumani, yakatifua vumbi ungedhani ni mashindano ya magari. Walifululiza moja kwa moja kupitia kwa baraste ya vichochoro kuelekea Mto Megwa.


Akiwa yeye ndiye aliyebebwa na aliye kiini cha safari hii,  Jera alijishughulisha na mbinu za kujitanzua. Itakuwaje? Kujifanya tu mfu hakutakuwa mwisho! Haya majanadume yanaweza yakampiga marisasi kadhaa. Alighadhabika kwa kushindwa kupata suluhu. Angejiokoa vipi kutoka mikononi mwa majambazi hawa?


Mara kwa ghafla, gari likapunguza kasi na kuegeshwa. Waliokuwa mle ndani walichomoka na kuanza kunong'onezana. Alijaribu kuyarefusha masikio yake asipate kusikia hata kidogo. Akajiweka tayari kwa pigano la maisha yake. Mwokozi wa maisha yake alikuwa nani kama si yeye? Alijiangalia mkononi na kutabasamu. Bahati gani aliyokuwa nayo! Hapo alihisi uwepo wa Mungu kwa kazi yake.


Walikuwa wamembeza kiasi cha hoja. Achukuliwe kama mateka kisha asifungwe? Walimwona vipi hawa? Kwani yeye hajiwezi? Alijicheka kwa kujiona duni. Mwanamume kama yeye kudharauliwa? La hasha! Angewafunza adabu hawa waliombeza.


Mara mlango ulipofunguliwa , Jera aliruka nje na hakuambiwa cha kufanya. Alimshambulia aliyeufungua mlango kwa mateke na mandondi mazito mazito. Kwa kuwa mwana mieleka hodari, alimfadhaisha adui wake. Akawa amepata kifungua kinywa asijue kishuka kilikuwa ki njiani chaja! Baada ya kumweza wa kwanza akajipa kwa wa pili na vivyo hivyo baada ya muda mfupi akawa amemfanyia yale yale aliyokuwa amemfanyia wa kwanza.


Akiwa mwenye furaha alijiona shujaa kwa kuwapiga majambazi wale. Kustaajabia alikuwa akipigiwa makofi na Shuta. Jera akatabasamu. "Heko kaka! Nimependezwa na mienendo yako ya kupigana! Hivi kwamba ulijifunzia wapi?" Shuta aliendelea kuropoka kama kasuku. Naye Jera kwa kushangaa akamtumbulia macho tu, asiseme lolote. "Wacha pia nami nione iwapo mafunzo yangu yalikuwa ya bandia kama ya hawa!" Shuta aliyasema haya huku akiruka kichwangomba hadi alikokuwa Jera. Jera akasonga nyuma . Akampima na kuona kuwa angempiga ngumi za haraka haraka afe naye aende zake kujishughulisha na upelelezi wake.


Jera akawa wa kwanza kukunja ngumi huku Shuta akimtazama kwa dharau. Jera alitayarisha mguu na ngumi kwa wakati mmoja akiwa na nia ya kumshtua na kumgonga mara moja. Alipovurumisha teke na kutupa ndondi mtawalia, alishangaa upeo wa kushangaa alipokutanisha mkonowe na ule wa Shuta. Teke alilokuwa amelituma shingoni mwa Jera likatekwa bakunja na kuinuliwa juu.

Kama hangekuwa amezoea mazoezi aina hii,  angepasuka msamba. Kwa vyovyote vile alijizatiti kumpiku Shuta. Ikawa yeye alikuwa anamfanyisha Shuta mazoezi kwa maana Shuta aliyakwepa mateke yake yote. Alipochoka akawa amemruhusu Shuta kuyatuma yake yaliyokuwa na uhakika na shabaha zaidi. Mengi yalimpata ilhali kunayo machache yaliyomkosa. Hata kwa yale yaliyomkosa yalimwumiza kiasi cha kufuja damu mdomoni na kipajini.


Jitu likasonga nyuma na kumpigia Jera makofi. Likacheka na kumwambia, "Nikimalizana na wewe nitamfanyia vivyo hivyo mpenzi wako. Itasemekana mliuana wenyewe kwa wenyewe."
Jera aliyapepesa macho yake kushoto akamwona Shauku amefungwa kwenye gari. Shauku akamlilia amsaidie. "Tafadhali nisaidie." Kilio cha Shauku kilimwondolea maumivu Jera akajikakamua kupigana. Alijipanga sawa sawa na kuyaamrisha makonde ya ufundi kumwangukia Shuta. Shuta aliona teke, akilihepa ndondi ya kooni ikampata sawa. Jera akamchangamkia Shuta. Akampiga sana hadi akadhani amemshinda nguvu alipoanguka.


Akamkimbilia Shauku na kumkata kamba. Akambusu. Akambeba na kumweka garini. Baada ya kuufunga mlango kwa nje, akajiona amenyanyuliwa juu na kutupwa chini. Angalikuwa hajasomea mieleka angalivunjika vipande. Ghafla kama umeme, akateremshiwa mateke mengi kwa mpigo. Mengi yakampata na akawa hana budi ila kutafuta hifadhi mtini. Wakawindana kama wanyama wa mwituni na walipopatana Jera akawa amepata kisiki.


Akakizungusha kisiki na kumtwanga nacho begani . Shuta alijisingizia kutosikia uchungu lakini mipigo ilipozidi ilibidi ajikune apatapo. Akawa amezidiwa maarifa. Hakuweza kuamini kuwa yeye pwagu alikuwa amempata pwaguzi.


Alipokuwa akiendelea kupigana na jitu, akasikia sauti ya Shauku ikionya, "Toka!" Alitazama na kuruka mbali akimwacha Shuta kubondwa na gari alilokuwa akiliendesha Shauku. Ukawa ndio mwisho wa Shuta.


Jera alimwangalia Shauku na kushangaa. Alikuwa amestaajabia ya Musa alipokuwa ametiwa mikononi mwa magaidi ilhali sasa aliyaona ya Firauni alipomwona Shauku akimgonga Jera kwa gari .


"Wewe ni nani?" Shauku aliulizwa. "Shauku!" Akajibu . "Yaonekana una mengi nisoyajua!" "Mengi kama yepi ?" "Mbona ukanifunga ?" "Kwa sababu nilitaka pesa." "Pesa? Pesa zikufanye umsaliti rafiki?" "Nilijua hakuna kingetokea. Nilikuwa nimekuona wewe si wa kuchezea!" "Alah! Ningeuawa ungefanya nini?" "Ingekuwa tu ni mojawapo ya bahati mbaya zilizowahi kunikumba!" "Huna utu!" "Una uhuru gani wa kunihukumu?" "Aliye na utu hamsaliti mie shujaa wa mdomo tu!" "Usidhani utanidanganya muda mrefu- najua wewe ni askari kanzu!" "Nani amesema?" "Hii hapa!"


Jera alionyeshwa mkanda wa kurekodi sauti akaingiziwa kwenye mkanda wa gari wa kucheza nyimbo. Alishangaa aliposikia akihojiwa moja kwa moja na Shauku. Kumbe Shauku alikuwa kachero! Mazingaombwe! Alijilaani kwa kumfikiria vibaya Shauku!


Lakini swali kuu likiwa aliporekodiwa alikuwa amepewa nini hadi akafichua siri kwa asiyemjua? Lazima angepata ukweli wa mambo! Aliapa!



TEGEA SEHEMU YA KUMI

Saturday, March 12, 2016

SEHEMU YA NANE

Ruzuku akiwa kwenye pilka pilka zake za hapa na pale shambani, alihisi malaika yakimsimama mwilini. Kisha mtima ukampapatika kwa kasi. Alitahadhari mapema na kuinama kuuchukua upanga aliokuwa ameuweka chini. Punde tu alipoinama mshale ukavurumishwa karibu kufumua fuvu lake la kichwa. Aliruka kulia na kuruka tena kushoto kila mara akiwa ameishikilia roho yake mkononi. Alitafuta hifadhi nyuma ya jabali na hapo ndipo alipochungulia na kuwaona washambulizi waliokuja kumvamia shambani mwa babake.


Alijaribu kuwatambua lakini kwake ilikuwa kama usiku wa giza. Hangeweza kuwang'amua kwa vyovyote vile kwani walikuwa wamevaliwa mabushuti nyusoni mwao. Ruzuku alipoona mavamizi yamezidi aliona vema kutumia ujanja ili kuwapiku mahasimu wake. Ni nani angemsaidia? Alimkumbuka dadake na kumhofia hali yake. Iwapo majanadume yenye misuli tinginya yalikuja kumtafuta kwa mapanga manene  manene sembuse kijisichana kidogo kama Zalza?


Aliliokota jiwe moja kubwa na kulivurumisha walikokuwa wavamizi. Sauti ya maumivu ilishamiri kote. Kumbe shabaha yake iliwajibikia jeraha kubwa lililokuwa kipajini pa mtu aliyekuwa chini akijigaragaza kwa maumivu. Kwa ujuzi na akili nyingi akaokota la pili na kulivurumisha upande wa kushoto. Hilo pia lilimpata mmoja wao shingoni, akaanguka chini na kuzimia. Akawa amebakia aliyekuwa kajihami kwa mishale. Je, angewezaje kujinasua katika mtego huu?


Alichora mpango, huku akiyakumbuka yote aliyoyapitia akiwa kikosini kule kambini mwa mafunzo ya kijeshi. Akiwa ghulamu staarabu hamna aliyemshuku hata kidogo licha ya kuwa nje kwa kipindi cha miaka miwili. Alipokuwa kambini, alikuwa amefunzwa namna ya kupambana dhidi ya adui yeyote. Akawa amefunzwa jinsi ya kupanga mipango ya kujitanzua bila ya papara.


Akiwa bado anakumbuka yale aliyofunzwa akamwona jambazi akiwa anamnyatia nyatu nyatu. Ghafla akakichukua kisiki kilichokuwa karibu naye na kwa shabaha ajabu akampiga mikononi adui yule. Podo ya mishale pamoja na mshale uliokuwa tayari kufumwa ukaanguka chini huku mwenyewe akikazana kumrushia Ruzuku makonde mazito mazito. Ruzuku aliyakwepa mengine na mengine yakampata. Akawewesuka na kupepesuka hadi chini. Ilikuwa wazi kwamba adui yake Ruzuku alikuwa mwepesi wa kutumia ndondi. Alimfuatanishia Ruzuku ngumi nzito nzito hadi Ruzuku akawa hoi. Licha ya kupigwa kama paka mnywa maziwa, Ruzuku alishangaa kuona akishindwa. Alijua tu ni mtu mmoja pekee ambaye aliijua mitindo yake ya kupigana; naye hakuwa mwingine bali rafikiye wa chanda na pete Salman. Ni yeye tu angemshinda vita.


Baada ya kujua mbona alikuwa anapigwa, Ruzuku aliyafumbua macho yake na kumsikiliza Salman akiongea kwenye simu tamba yake. "Kazi ishaisha …" alidai.  "Kongole kwa kuifanya kistaarabu " Alipongezwa. "Ni wapi nitaizika mizoga yao?" Aliuliza. "Fanya vile utaamua." Aliambiwa. Kile hakufahamu ni kuwa Ruzuku alikuwa ashamnyemelea nyuma kwa nyuma alipokuwa akiongea kwa simu. Ruzuku alimpiga ngumi moja ilimwondolea fahamu kwa muda kiasi. Akamyang'anya bushuti. Alishangaa upeo wa  kushangaa alipouona uso wa Salman



Alimgaragaza kwa kumpiga mandondi mazito mazito. Akamwuliza maswali  lakini hakupata hata robo ya majibu. "Mbona unataka kunimaliza?" "Ulitumwa na nani?"
"Umefanya mauaji mangapi tangu tulipowachana?"


Ingawa Salman hangependa kufichua siri ,hakujua kitini alimokalia kulikuwa na miale ya aina yake ya tarakilishi iliyokuwa ikizisoma akili  zake Salman. Bila kujua akawa ameyarekodi yote aliyoyafikiria siku hiyo.










TEGEA UHONDO WA SEHEMU YA TISA UONE JINSI MAMBO YALIGEUKA YAKAWA SHUBIRI. JE SALMAN ATAJINASUA KIBINDONI MWA RUZUKU?

Tuesday, February 9, 2016

SEHEMU YA SABA

Jera aliamka akiwa hoi bin hoi. Matukio ya mkesha wa usiku huo yakiwa yamemsakama koo asiweze kujielewa. Alihisi kuwa mzito ajabu. Shingo yake ikiwa na maumivu tele, alishindwa kuelewa ni nini kilichomtatiza. Alichojua tu ni msichana aliyekuwa naye usiku hakuwepo. Jina lake nani? Hakumbuki …  Jera akajipa moyo akidhani labda ameenda hamamu kuoga. Jina la huyu kipusa likamchezea shere, lisiweze kujiandikisha akilini mwake.Kila akijaribu kulikumbuka akajiona kizani. Maumivu yakamtwika hasira akawa basi hana budi ila kumlaani msichana yule.


Ikawa akiwa katika hali hii ya hasira, akausikia mlango ukifunguliwa kwa utaratibu. Hisia fulani ndani mwake zilimwelekeza aamke na kuchukua silaha ilhali nyingine ikapinga hoja hiyo. Alipojaribu kuamka akajipata amefungwa ndi asiweze kuinua hata kichwa. Alijaribu kujikwamua lakini wapi! Juhudi zake ziliambulia patupu… Jera akajua basi yu mtegoni na kwa hivyo akaamua kuwa yoyote ambayo yangetokea hangeufichua ukweli wowote kumhusu na alichonuia kufanya. Akakata kauli kuhepa tu punde atakapopata upenyu. Kufikia sasa akaelewa ukweli wa msemo Zimwi likujualo halikuli likakumaliza.


Akiwa mwepesi wa kufikiri, alitumia ujanja na kujifanya mahututi alipousikia mlango wa ndani ukifunguka. Alisikia minung'uno ya wanaume wawili na mwanamke mmoja. Alijaribu kujiuliza ni wapi alikuwa amewasikia watu hao lakini akili zake zilimwasi. Katu hangetambua kuwa mwanamke ni Shauku na wanaume wawili ni Chonde Kipofu na mlinzi wake, Shuta.


"Unadhani huyu ni mpelelezi?" Shauku akataka kujua. "La hasha!  Huyu si mpelelezi bali ni mdokozi… Itakuwaje aulizieulizie kila amwonaye kunihusu?" Chonde akatamka. "Kama anauliziaulizia habari za kwako, hudhani ni tisho kwako? Je, hizo habari yuataka kuzipeleka wapi au ni nani aliyemtuma?" Shuta akawa mwepesi wa kuuliza. "Mimi kazi rahisi nishawapa nyie. Ndovu nishamweka chini. Mlinituma kumwinda- ndio huyu hapa… basi za kwangu nigawie." Shauku akatamka. "Mbona haraka hivyo? Ama umetutega hapa tulipuke pindi tu tutakapokupa pesa zako?" Chonde akataka kujua. "Alaah! Si bado nitakuwa ningali hapa kumaanisha kwamba nitalipuka nanyi …" Shauku akajitetea na kisha akaongeza, "sikujua pia adinasi kama nyinyi huogopa kifo." "Hamna asiyeogopa kifo… kwani kifo njia ya kila mja." Shuta akasema. "Mhesabie vidonge vyake huyu dada kisha umpe halafu … huyu jamaa mkamtupe mtoni afie kuko huko. Hana umuhimu wowote ule kwa kikosi." Chonde akadai. "Lakini Bwa'mkubwa si tulielewana kifo cha Azenge ndicho kitakachokuwa cha mwisho kutekeleza?" Shauku akauliza moyo ukimpapatika kifuani.


"Shida yako nini? Ulitaka pesa-ndio hizo dada…utanifanyia kazi hadi utakapokufa na mshahara utapata maradufu …" Chonde akamwambia wazi. "Nishafanya mengi mkubwa ninachoomba ni kutotekeleza mauaji mengine kando na yale nishatekeleza." "Umeanza kumea pembe! Ni sharti utambue kupanda mchongoma si kazi …" "Lakini mkubwa …" "Sizitaki lakini zako…" "Mie nishasema…" "Useme usiseme lazima utafanya ulichoamua kukifanya- lazima ufanye majukumu yako bi'mdogo…" "Ukitaka niwachane na kikosi nitafanya hivyo tu bila kusita…" "Utakufa…" "Nitakufa nikiwa nimefurahi angalau sijalazimishwa kufanya lolote kama ilivyo desturi yangu…" "Unakaidi kiapo ulichokula…" "Haitakuwa mara yangu ya kwanza kukaidi!" "Una haki gani? Una haki gani kuniongelesha namna hii?" "Aliyeanzisha mabishano ni nani?" "Wewe hapa! …" "Kiini chake kikiwa nini? Mauaji? Basi jua siogopi kufa-kufa kwa mwili sio kufa kwa mtima… angalau jamaa wangu watajua nilikufa nikitetea moyo wangu walioujua tokea jadi…" "Utundu haulipi!" "Kwani umewahi kusadiki maana yake?"


Shuta alikuwa tayari kumwelekezea Shauku bastola iwapo Chonde angemruhusu. Alikanyaga kanyaga sakafu kwa hasira alipoona vile mwajiri wake alipokuwa akibezwa na kijanajike. Hakuamini aliyokuwa akiyasikia. Iweje mwajiri amruhusu mwajiriwa kumkunja kunja kiakili? Alitaka kukifunza hiki kijisichana umuhimu wa adabu lakini alihofia maamuzi ya Chonde. Kwa kujitambua na kutanua kifua chake kwa majitapo, akamwambia Chonde, "Wacha apigane nami , akinishinda basi atakuwa huru kufanya lolote alitakalo…"
"Ni makosa uyafanyayo Shuta. Usimdharau kiasi hicho…"
"Simdharau bali ningependa sana kumfunza taaluma ya adabu. Hawezi akamkosea mkubwa wangu heshima nami nikae tu… anipige asiponipiga nimpige …"
"La hasha!"


Jera alijisingizia kutokuwa na ufahamu. Hata alipomsikia Shuta akimwomba Chonde nafasi ya kumfunza adabu Shauku alishikilia roho mkononi akijua Shauku angenyanyuliwa mbawa kama kuku aliyechinjwa. Licha ya Shauku kumkosea, alijipata kumpenda na kumwonea huruma alipokuwa akilazimishwa kuua tena. Angefanya kila awezalo kumnasua Shauku kutoka mikononi mwa jitu hili kwa vyovyote vile. Alijiahidi. Mtiririko wake wa mawazo ulikatizwa na sauti nene ya Chonde ikipeana amri. "Mfungue huyu kisha mkamtupe kule msituni akiwa amefungiliwa mtini . Hakikisha hakuna anayemwona."


Jera akajua mtihani wake mgumu ni kujifanya mfu ndiposa aweze kuhepa ikiwezekana. Basi wakavaa mzima mzima na kumtupa ndani mwa gari na kwa kasi wakafululiza hadi walikoambiwa. Jera ,.akijua amo kazini akawaza na kuwazua cha kufanya. Alijiona mnyonge kama unyoya unaopeperushwa angani kwa nguvu zisizo zake.







TEGEA SEHEMU YA NANE


Monday, February 1, 2016

SEHEMU YA SITA

Zalza hakuamini kuwa alikuwa kabaki yatima. Kaka yake, Ruzuku, alikuwa ndiye tu mtu wa aila yake aliyekuwepo. Wote katika familia hii walikumbatiwa na mauti wasiweze kubanduka. Aliamka toka alikokuwa ameketi na kujinyoosha. Alipiga miayo na kupiga chafya mara kadha. Akidhani ni uchovu na kibaridi kilichoshamiri kote, akajifunika kwa blanketi lake zito. Mara akaanza kuhisi joto kali. Akalitupa blanketi lake kando na kuamka. Alikuwa amelowa chepechepe kwa jasho lake mwenyewe.

Mtima ulimpapatika kwa kasi. Damu yake ikiwa moto ajabu ikamfanya atafute maji ya kujimwagilia. Punde tu aliposimama, alihisi kizunguzungu na kuanguka sakafuni pu... Aliona giza likimvamia na hakuweza kufanya lolote kulihusu giza hilo. Likamteka nyara. Akazimia.

Hakujua alikuwa mfu kwa muda  gani lakini alipojisikia nafuu, alijiona ndani mwa nyumba asiyoifahamu. Ilikuwa imeezekwa kwa nyasi. Kuta zake zikiwa za matope ziliogofya. Michoro ya aina aina ilisheheni kuta zote. Zalza alitamani kuamka lakini akashindwa. Shingo yake ilihisi maumivu makali kisha kichwa kikaanza kumuwanga. Katika hali hii, Zalza alijifisha angali hai. Akaonekana mnyonge. Akawacha machozi yampukutike njia mbili mbili.


Baada ya muda mchache, akajaribu kupangusa machozi yake lakini alistaajabia ya Musa alipotanabahi mikono yake ilikuwa imefungwa kwa kamba na alipozidi kugutuka mlango wa ulifunguka.


Mwangaza uliopenyeza mlangoni ulikuwa wa kupofusha macho. Zalza akayafumba macho yake na baada ya muda akayafumbua. "Nafurahia kukuona u mzima!" Sauti ya mwanamume ikasikika. Fikirani mwa Zalza alihisi kana kwamba amewahi kuisikia sauti hiyo mahali. Akajitesa kujikumbusha ni wapi alipoisikia sauti hiyo. "Naona unajibidiisha kutambua ni wapi uliponisikia nikiongea kabla ya hapa. Hivyo ni vema. Inaonyesha kweli umeamka." Sauti iliendelea kumtesa Zalza. Alizikumbuka sauti za watu wengi lakini hakuna iliyofanana na ile aliyokuwa akiisikia chumbani mle. "Zalza, tuseme hunijui?" Sauti iliuliza.


Ghafla bin vuu Zalza alitambua mwenye sauti na kwa uchungu akamwuliza, "Ni nani asiyekujua Wewe? Ni nani asiyekujua wewe Subabi, mtoto wa  Ngaruhi?" "Heko kwa kunijua! Hivi sasa sina shaka unajua kiini cha swala kuu…!" "Swala kuu?" Zalza akamchachawiza. "Ndio. Swala nyeti. Hivi tuseme unanipenda ama bado wanichukia?" "Ni nani anakuchukia? Sina sababu yoyote ya kukuchukia …" "Basi mbona hunipendi? Nimekuongekesha na kukubembeleza kiasi cha haja ila kwako hunioni mimi. Wewe humwona Shara tu! "Yafaa ujue kwamba hamna siku utakayolazimisha mapenzi. Mapenzi hayahitaji shurutisho lolote ndiposa yamee na kukua. Mapenzi huota tu yanapostarehe kuliko na rutuba. Hivi utanichukia kimakosa tu. Tabia zako ndizo zitakazokukosesha mke. Badili tabia nawe utaogelea katika bahari mapenzi …" "Ati? Nibadili tabia gani?" "Yanishangaza eti kuwa wewe mwenyewe huzijui tabia za kwako. Hujui kuwa wewe huoa kila wiki- kila juma na mke tofauti? Hujui?" "Eeeh! Lakini mie nakupenda Zalza…" "Unanipenda? Hebu rudia tena?" "Unanipenda? Unanipenda kisha wanifunga kwa kitanda? Ni nani atakayempenda mtu kisha amtie taabu aina hii?" "Nilikufunga kwa kuwa nilihofia ungetoroka…" "Kumbuka tu nishakuambia mara nyingi kuwa mimi si wa aina yako! Sikupendi na hakuna siku nitakayokupenda!" "Hutapenda nitakayokufanyia ukizidi kuwa mkia wa mbuzi …" "Sitapenda? Ni kama kuniambia nimependa ulivyonifunga kama mfungwa!" "Basi sina budi kumfanyia kazi aliyenituma…" "Haina haja ya kujifanya. Maliza ulichoanzisha na ukumbuke kumpenda anayekupenda ni mapenzi ila kumpenda asiyekupenda ni ubatili…" "Falsafa zako zipelekee Shari. Kabla ya kukupeleka huko kwa mwajiri wangu lazima nikuchune…" "Ninajua unapenda kufanya hivyo na hata maongezi haya yalikuwa yanakuchelewesha. Njoo ufanye upendavyo lakini ujue  Ruzuku akijua tu ulichokifanya atakung'oa macho!"




"Hunitishi mimi… Nilisahau kukutaarifu kuwa labda pia yeye amefanyiwa vivi hivi ulivyofanyiwa wewe…" "Sizitaki taarifa zako Subabi…" Maongezi haya yalishika moto yasiweze kukoma. Zalza alimkumbuka Kuwili na akajihurumia. Dunia duara huenda yaliyomfika mwenzako yakakufika na wewe. Daima dunia haikosi maajabu. Subabi aliufikia mshipi wake na kuufungua. Kisha akaiteremsha suruali yake ndefu hadi magotini. Akaugusa gusa uume wake na kuusimamisha. Akamwangalia Zalza kwa dharau na kumwambia, "Ulichoninyima kwa miaka sasa nimekipata bure bila kupiga bei…" "Nishakuambia gharama yake. Macho yako mawili yatang'olewa na kakangu mkubwa …" "Vitisho baridi haviniachishi uchu wa kukusimika uume wangu." "Tahadhari kabla ya hatari…" "Usipohatarisha ni nini utatahadhari?" "Mwisho wako nauona…" Labda ungeona mwanzo ndio ningeshtuka. Nikikupeana kwa mkubwa wangu, nitakuwa nimeshiba. Nitakuwa nimeshiba utamu wa mapenzi yako…"


Zalza alikata tamaa asijue cha kufanya. Akamwona Kuwili na yaliyomfika. Akajua wembe ni uleule, hatima ni ileile na maisha ni yaleyale ; yalivyokuja ndivyo atakavyoyaishi. Akamwangalia Subabi machoni na kumwambia, "Nyinyi watovu wa nidhamu mtaona kilichomng'oa kanga manyoa. Wewe pamoja na yule aliyekutuma mtaona giza palipo na mwangaza…" "Mimi nitakuwa nimekuonja naye mkubwa wangu atakuwa amekuchovya utamu wote…" Zalza akijua maisha yake yamo hatarini alitaka  kurefusha mazungumzo akiwa na matumaini ya kuokolewa kutokana na dhiki hii. "Haha…!" alijitia kicheko, "Na huyu bwana mkubwa ni nani? Mbona usimtaje jina?" "Sheria yetu haituruhusu tumwite jina…" "Sheria? Msiniambie pia nyinyi hufuata sheria?" "Mbona tusifuate?" "Hivi kwamba mna sheria? Na unatii hiyo sheria? Mbona nauona kama ubatili?" "Ki vipi?" "Iweje unafuata sheria na huku sheria yenyewe inapinga utekaji nyara na ubakaji?" "Kimya!" Alifoka Subabi huku macho yakiwaka kwa hasira.
"Najua unataka kuahirisha hatima yako- kumbuka kuwa siku ya nyani kufa miti yote huteleza…"




Subabi akiwa ameshikwa na ashiki, aliitoa chupi yake na kuanza kumvua nguo Zalza. Zalza akijua chuma chake ki motoni, akapaza sauti kwa nguvu zake zote. Alishangaa aliposikia sauti yake ikimrudia. "Wanadamu hawakai huku. Tuko mbali sana. Utamaliza nguvu zako bure badala ya kuzifanyia kazi nzuri kama ya kupokea na kunitunuku utamu wako wote!"  "Mende wewe!" "Mende huyo atakuonja leo."



Alipomaliza kumvua nguo aliipanua miguu yake. Akatema mate kiganjani mwake na kumpaka jogoo wake. Aliinama na kumlalia Zalza kisha kwa kwa nguvu akajaribu kupenyeza mle ndani. Hakuweza kuingia. Licha ya kubisha sana, mlango haukufunguka. Alipoinamisha kichwa chake atazame abishako, mara Zalza akamng'ata shavu. Alijaribu kujing'atua lakini wapi! Aliamua kutumia nguvu akijua kuwa daima dawa ya moto ni moto. Subabi  alimpiga ndondi ya tumbo na hapo Zalza akamwachilia. "Hiyo alama haitawahi futika." "Pia hii yenye nakutia haitawahi futika!" Alimjibu. Subabi akiwa amemfunga Zalza miguu aliufungua mmoja na kuufunga karibu na kichwa chake. Kisha akaufungua ule mwingine na kuufunga upande ule mwingine. Akawa amepanua njia. Zalza akiwa amejaribu kadri ya uwezo wake na kushindwa kujikwamua kutokana na Subabi akakata tamaa. Liwe liwalo ataishi akijua hakukuwa kupenda kwake. Hakumsumbua Subabi alipokuwa anaingia. Subabi akaiingia akafanya yote aliyohisi yalimfaa. Hakutosheka haraka alimtendea Zalza yasiyoweza kusimuliwa zaidi ya hapa. Kisha akimcheka Zalza na kumbusu ziwani. Alijua kazi yake ishaisha na iliyobaki ni kumsafirisha Zalza hadi kwa mkubwa wake.

TEGEA SEHEMU YA SABA

Wednesday, January 13, 2016

SEHEMU YA TANO

Ruzuku hakuamini macho yake alipouona mwili wa baba yake ukiwa pale ukumbini. Aliutikisa kwa hamaki, akilia kwa uchungu mwingi. Machozi yakamtoka njia nne nne naye pasi kujielewa, akaendelea kulia huku wimbo wake ukisheheni kote.

"Ni juzi tu ulinibusu,
Ukaniahidi utanipa zawadi,
Kwa kupita mtihani ungenipeleka shule,
Mbona hivi sasa?

Mbona mauti hauna heshima?
Mbona hauna huruma?
Mwaka haujatamatika ulipomchukua mamangu,
Mbona usishibe naye?

Tumaini letu ushatunyang'anya,
Zalza angali mchanga,
Mbona mchanga ukubali kuwameza wote tuliowaenzi?
Ni nini tulichowakosea hadi wazazi mkatunyang'anya?

Kafara gani tuitoe,
Machozi yametulowa,
Ni dhahiri tunapagawa,
Msingi wetu ni dhaifu,
Ni nani atatujali,
Maskini Mayatima wa Mungu'



Ruzuku alijililia hadi usingizi ukambeba. Alimwona baba yake akimtania. Akacheka. "Nikuulize mwanangu, hili jina lako Ruzuku ni gari la kuenda wapi?" Baba mtu akamwuliza huku akicheka. "Hivi unataka kunipanda twende wapi?" Ruzuku akazidi kumtekenya babake. "Ala! Hili gari halistahilimili uzito wangu mie Mwaga wa Nziva!" Babake akamchekelea. Ruzuku akamchokoza babake, "Na aliyekupa jina Mwaga alikusudia nini? Kwani wewe mwoga? Ama alishindwa kutamka mwaka?" Akaangua kicheko alipomwona babake akiinamisha kichwa asishindwe kujitetea. Haya mazungumzo hayakunuka ukale fikirani mwa Ruzuku. Ingawa yalikuwa yamefanyika kitambo kidogo, aliyaona kama ya sasa. Tabasamu la baba yake likazidi kumbeza ni kana kwamba kumwambia "Hukunihifadhi vema nilipokuwa nikiutanua usowe babako. Kwa sasa hadi milele hutoniona mie wala baba yako. Kula ujeuri wako!"


Alipozinduka kulikuwa kumekucha. Akaangaza macho alikolala na kuona damu nyingi ikiwa imetapakaa kote. Alishtuka akidhani ni damu yake iliyomwagika sakafuni. Akapaza sauti kumwita dadake. Zalza alipowasili hakupewa mapumziko bali alirushiwa maswali mazito moja baada ya jingine . "Nieleze kinaganaga ni yapi yalikuwa yametokea kabla ya baba kukutuma mwituni?" "Kuna mzee fulani mkubwa kwa serikali aliyekuja hapa kupiga gumzo na baba! Walizungumza sana wakicheka ila nilipomtazama baba kicheko chake hakikuwa cha kawaida! Labda alijitia kufurahia kile alichoambiwa!" Zalza akamjibu Ruzuku. "Baba alikuzungumzia baada ya hapo? Alikufahamisha kiini cha mazungumzo hayo?" Ruzuku akauliza. "La hasha! Aliniambia tu jina la kiongozi huyo. Jina lake Chonde sijui Kipofu ama Kibovu " Ruzuku akajuzwa. "Mbona basi akakutuma? Unaweza kukumbuka maneno yake yote aliyokutuma kuniambia?" Ruzuku akataka kufahamu.


"Nenda mwituni alikoenda Ruzuku. Mwambie huku si kwema kama yalivyo mazoea…" Zalza akaelezea jinsi alivyoambiwa. "Hayo tu?" Akachachawizwa. Kwa upole Zalza akaelezea yote. Kufikia hapo ndipo Ruzuku alipoelewa mazungumzo ya baba yake na Chonde ndiyo yaliyochangia kifo alichokufa babake. Wangefanya nini wala wangetenda nini?


Mazishi yaliandaliwa na Mzee Mwaga akasafirishwa kuenda nchi za wafu. Wote waliohudhuria mazishi waliwaonea huruma kina Ruzuku lakini walipofumukana kunao waliosherehekea kifo cha Mzee Mwaga. Hawa walikuwa wafuasi wa Chonde Kipofu. Walijua sasa shamba la Mwaga lingechukuliwa na Chonde nao kugawiwa. Ndio kwa maana kila siku walikesha kwake. Hata Chonde hakufahamu walichopenda watu hawa ; pesa na mali yake au yeye mwenyewe. Hakuwa na chanzo cha kuwashuku kwa hivyo akalitumbukiza swala hilo katika kapu la sahau kama alivyomtumbukiza Mzee Mwaga kaburini.

Tegea sehemu ya sita 

Tuesday, January 12, 2016

SEHEMU YA NNE

Jera alifungua mlango wake kisha akaukomelea kwa ndani. Akajishika
tama asiweze kujua pa kuanzia. Baada ya muda mchache akajirusha kwenye
kochi lake. Chumba chake kilikuwa kikubwa kiasi cha hoja. Maadamu kina
uwezo wa kuchukua makochi manne, kabati na kitanda basi angetaka nini
zaidi mseja kama yeye?




Aliamka pale kochini akajiendea zake hadi kitandani. Akajitwaa pale
huku amekibeba kichwa chake viganjani mwake. Labda kazi aliyokuwa nayo
ndiyo iliyomkosesha starehe. Akachukua kicha cha funguo na kuzikagua.
Akachagua ufunguo mmoja mdogo na kuinama. Kisha akaupenyeza ubavuni pa
kitanda. Ghafla kukatokea kijilango cha saraka ya kitanda. Mle ndani
mlikuwa na ala zote za vita alizohisi muhimu kwake.




Akachukua bastola moja nyeusi aina ya Triple Round akaipangusa kutoa
vumbi. Kisha akaijaliza mfuko wa marisasi. Alipomaliza kuikagua,
akatabasamu na kucheka kicheko ambacho hakikumtoka vema.




Jera alipoangalia kushoto alishtuka kuliona jitu moja nene likiwa na
silaha hatari mkononi. Akachupa kulia na kubingiria kwenye sakafu
akitafuta hifadhi kabla hajakabiliana na jitu hilo. Alijificha nyuma
ya pazia lililogawa chumba hiki kumngojea hayawani yule. Akasubiri kwa
takribani nusu dakika asiweze kumwona au kumsikia yeyote akitembea.
Kile alichosikia ni mdundo wa moyo wake uliomtisha hata yeye mwenyewe.




Jera akajitia ujasiri na kuondoka aste aste kuelekea alikomwona mtu
yule. Akapita pale alipokuwa lakini hakumwona yeyote. Akadhani ni
fikra tu ndizo zilizomkabili. Ghafla bila simile, alipoelekeza macho
yake kushoto akamwona mtu huyo. Akachuchuma kutafuta hifadhi naye vile
vile akachuchuma. Akakichukua kisu na kukitupa kuelekeza ubavuni mwa
kushoto mwa mtu huyo. Naye vile vile akakitupa chake kumdunga Jera.
Kutanabahi kioo kilichokuwa mbele zake Jera kikavunjika na kuwa vigae
vigae.




Alipangusa kijasho chembamba kilichomtiririka usoni na hanchifu yake.
Akajicheka kicheko dhaifu. Akamaizi kuwa licha ya visa vya ushujaa
wake kuenea kote kama moto wa nyikani alikuwa mwoga kupindukia.
Alienda kwa meza. Akamtazama mtu aliyekuwa ndani mwa kioo cha meza na
kumfananisha na jambazi aliyemwona.




Jera akapasua anga kwa kuangua kicheko kikubwa ajabu. Hakuweza kuamini
kuwa yule aliyemwona ilikuwa picha yake kwenye kioo. Alipokuwa bado
anajicheka na kujifedhehesha hivyo, aliusikia mgoto kwenye mlango
wake. Akafanya pupa kuiweka bastola yake na ala nyinginezo sarakani na
kuifunga.




Kisha akaufungua mlango. Jera alitabasamu alipomwona Shauku, msichana
mrembo akimtaka radhi kwa kuchelewa. Alikuwa mrefu wastani na mwenye
umbo la kupendeza. Nywele zake zikipimwa urefu kila kuchao zilimfanya
aonekane mchanga. Shauku akamwangalia Jera usoni.




"Hukaribishi wageni?" akamwuliza.
"Nilikuwa bado najishibisha urembo wako." Jera akajibu kwa utani.
"Wacha porojo zako. Wewe nikaribishe niingie."Shauku akasema. "Mtu
hakaribishwi kwake." Akajitetea Jera. "Kichwa cha kuku hakistahimili
kilemba..." Shauku akamdokezea Jera japo kwa kusitasita. "Wewe yawache
ya kuku uingie kwako ustarehe. Hujui kwamba lisemwalo lipo na kama
halipo li njiani?" Akamwondolea wahaka.




Walitazamana, wakatabasamu kisha wakapigana pambaja; kila mmoja akiwa
na mengi ya kusema. Shauku akiwa Mwana dada mrembo hakuwa mgeni wa
ulaghai. Alijua jinsi watu huwalaghai wenzao hasa wanaume
wanapowashibisha vidosho wao kwa maneno matamu wakiwa mawindoni na
punde tu wanapowaringa hutoroka. Alijifunza mengi asijue Dunia bahari
ya mafunzo. Akidhani ameerevuka akajipa pumbavu; mwehu wa kupindukia
kana kwamba hakuwahi yapitia hayo.




Aliyakumbuka yote aliyoyapitia; mema kwa mabaya. Mabaya yakiyapiku
mema. Akiwa amemaliza masomo yake ya kidato cha nne akampata Navila
aliyemzindua na kumtia ulimbo na kumnata akilini. Akawa hoi wa
mapenzi; hakataziki. Tamati gonjwa la zanaa likamteketeza. Bahati ya
Mungu akapona.




Akapachikwa doa la mapenzi akiwa chuoni. Akidhani amewahi katika
ulimwengu wa mapenzi Jolada akamringa na kutokomea kusikojulikana.
Alijaribu juu na chini hadi akalea mimba yake japo kuna marafiki zake
waliompa wasia wa kuavya mimba. Wakimwambia jinsi kumlea mwana ni
gharama na kwa upendo wao wangemlinda endapo angepata shida yoyote,
Shauku aliuona kama ubatili wa hali ya juu. Ubatili wa mapenzi ambao
kamwe haungemkosesha raha ya kuitwa mama. Akamzaa Isa, kifungua mimba
wake.




Akiwa amekula kiapo kutopenda mwingine kwa dhati kama mwanzoni
akajipata mikononi mwa Jera, mwanamume mcheshi, mstaarabu na mpenda
amani. Angeweza kumkataa Jera? Angeweza kuufungua moyo wake kwa
kupenda tena? Kiapo alichokula cha kuwahadaa na kuwahangaisha wanaume
kingevunjika? Na iwapo kingevunjika, kitamdhuru kweli? Akajihurumisha
kwa maswali chungu nzima. Kufumba na kufumbua akajiona amebebwa mzima
mzima hadi kwenye kochi. Shauku akamwangalia Jera na kutonesha chozi.
Hakujua kuyatoa ya mamba lakini yakiwa ya ubatili yalimbubujika njia
nne nne asiweze kuhimili na kuhisi mabusu yake Jera mwilini kote.





TEGEA SEHEMU YA TANO

Friday, January 8, 2016

SEHEMU YA TATU

Zalza alizidi kutamaushwa na kumbukizi zilizotua na kupanga makazi
fikirani mwake. Katu hangeweza kutembea upesi kwani hata nayo miguu
yake ilitamani kuyajua yale yaliyomfikirisha. Akawa hoi. Akasahau
alikotumwa. Akasau umuhimu wa safari yake.




Alipokuwa akipumzika, ghafla kulitokea mngurumo wa kutisha. Akajirusha
juu. Kwa bahati akauparamia mti wenye matagaa kila upande. Akajisetiri
matawini asionekane. Mara kukatoea simba mkubwa ajabu. Alikitikisa
kichwa chake kisha akaanza kusonga mbele.




Mwili ulimkandamana Zalza; asijue cha kufanya. Aliyakodoa macho yake
pima ungedhani gololi. Uhai wake wote nusura umwagike. Kisha akamwona
msasi aliyekuwa na vifaa vingi vya kuwinda. Akidhani angalau msaada
ulikuwa tayari, akampigia mluzi; ishara kwamba amemwona. Msasi
alipofahamu kulikotoka mbinja, akautoa upanga mshipini pake. Akaanza
kuukata mti huo. Hofu ikamwingia Zalza. Akaamua kupiga unyende mkali
wa kumkatisha maiti usingizi wake wa pono.




Kila Zalza alipojaribu kutafuta msaada, mwangwi ulimjibu. Akawa ni
kana kwamba anayejibeza. Huyu kijana mtoro anayependa kuwafanyia watu
mzaha alitoka wapi? Baba yake ni nani? Ana akili timamu? Mbona kila
anapoita yeye huita? Mbona yeye huyaiga maneno yangu? Haya maswali
yalimtanda Zalza mithili ya utandu wa buibui. Akawa hoi bin hoi;
asijimudu kwa lolote.




Alipogutuka mti ukaanza kuyumba yumba ishara kwamba yeye Zalza alikuwa
matatani. Je, ni nani asiyejua kuwa mti mkuu ukivunjika wana wa ndege
huyumba yumba?




Zalza alipoona mti ukielekea chini alipaaza sauti ya haja kisha
akafungua macho. Alitarajia kujiona chini, amevunjika vipande vipande
ama akiliwa na simba wa msasi. Yote hayo hayakunaswa na mboni zake.
Alipojielewa, alijihisi amerowa chepechepe labda kwa mkojo au kwa
jasho la uoga.




Akapepesa pepesa macho yake kila upande asimwone simba aliyetaka kumla
wala kumwona msasi mwenye kufuga simba. Akaupanua mdomo wake kisha
akaubana. Yote aliyaona kama mazingaombwe.




Alipojielewa, alifululiza njia hadi alikotumwa. Akiwa mwepesi ajabu
aliruka vichaka vilivyofanya viunzi njiani na kutoka shoti. Alimkuta
kakaye, Ruzuku, akipasua kuni. Hakungoja hata sekunde ipite kabla
hajamjuza yaliyomleta hapo.




Ruzuku alipoyasikia yale aliyofahamishwa alikata kauli kuwa lile jambo
lilikuwa la dharura na angejibidiisha mpaka afike kwao.




Akafunga kuni alizokuwa amezipasua kisha kuzitundika begani.
Akamwangalia dadake na kwa ishara waliyoelewana wao kwa wao wakang'oa
nanga kurudi kwao.




Akiwa mwana riadha shupavu, Ruzuku hakuchoshwa na mzigo alioubeba.
Aliuona mwepesi. Akajizatiti kuongeza mbio. Kwa mteremko akijiwachilia
kama unyoya wa kuku na mlimani akipanda kama gari lililowekewa injini
ya ndege.





Zalza akaanza kuhema, kutweta na kutoa pumzi kwa taabu. Mbio za Zalza
zikapungua. Akamwangalia kakake. Ruzuku naye akasita. Akaliangalia
tita la kuni alilokuwa amelibeba.




Pendo la ndugu wa toka nitoke likatawala. Akalitupa tita lake la kuni
na kumchukua kijeshi mnuna wake. Akaendelea na papara zake za kufika
nyumbani mapema. Zalza naye kinywa wazi asijue aliko wala aendako.
Mate yakimtiririka mdomoni.




Punde tu alipofika karibu na nyumba iliyokuwa mkabala na shamba lao
akasikia ukelele mkubwa wa watu waliojawa na ghadhabu.




Yeye kwa kutojua yaliyokuwa mbeleni akaendelea na mbio zake. Hatimaye
mbio zake zilifika ukingoni alipoonekana. Wakijua ndiye mwizi wa
wasichana kijijini wakamvamia wasijue wanamvamia mtu na dadake na
kumwacha mwenye kosa kutorokea wasikojua. Kufumba na kufumbua, Ruzuku
akawa mahututi kwa kupigwa kama mbwa aliyeingia msikitini.




Wanakijiji walipotambua kile kichotokea ndipo walipomwandalia huduma
ya kwanza na baadaye kumpeleka kwenye zahanati iliyokuwa karibu.
Waliobaki waliendeleza shughuli ya kumsaka mwizi aliyeponea tundu la
sindano. Ikawa mara yake ya kumi kuiba na kuhepa na wasichana kumi na
wawili.




Baada ya kupokea matibabu na fahamu zote kumrudia, Ruzuku alianza
kujielewa. Hata akakumbuka ni wapi alipokuwa kabla ya kuvamiwa.
Akakumbuka ni wapi alipotakiwa kuenda upesi.




Kutahamaki Ruzuku akajitoa mifereji ya damu na maji na kutoroka
hospitalini. Alifululiza moja kwa moja hadi kwao. Akapata mwangaza
mkubwa ukiwa umezagaa kote. Akaingia bila kubisha. Hakumwona yeyote.
"Baba?" Akaita. Ghafla tu alipomwita babake kukatokea vilio vya ajabu.
Wengine wakimsifu mwenda zake kwa ukarimu wake ilhali wengine
wakiusifia ujasiri wake baba mtu. Ruzuku akalengwa lengwa na machozi
huku hasira zikimtania. Akawa hana budi kusadiki kuwa baba yake
alikuwa amesafiri jongomeo pasi kumbariki...



Tegea Sehemu ya Nne ujue jinsi mambo yalivyoendelea. Asante kwa
kukisoma kijisehemu hiki. Iwapo una maoni ya kujenga au kubomoa au ya
kuongezea unao uhuru wa kuyatoa katika kijisanduku cha
maoni(COMMENTBOX) hapa chini. Shukrani